Wenyeji wa mtaa wa Owino Uhuru eneo bunge al Jomvu kaunti ya Mombasa wamesema wataendelea kukita kambi nje ya majengo ya mahakama ya Rufaa mjini humo wakisema hawataondoka hadi kesi yao itakapoamuliwa na waathiriwa kufidiwa.
Hii ni licha ya mahakama hiyo ya Rufaa kuhairisha tarehe ya kutoa uamuzi dhidi ya fidia ya shilingi bilioni 1.3 kwa zaidi ya wenyeji elfu 3 wa mtaa wa mabanda wa Owino Uhuru ambao waliathiriwa na kemikali ya Lead.
Katika barua kutoka kwa msaidizi wa msajili wa mahakama hiyo uamuzi huo ambao ulipaswa kutolewa leo Ijumaa umeahirishwa hadi tarehe 14 mwezi ujao wa Apili na kulingana na mkurugenzi mkuu wa shirika lisilokuwa la serikali la Haki na masuala la mazingira la CENTER FOR JUSTICE GOVERNANCE AND ENVIRONMENTAL ACTION Phylis Omido amesema zaidi ya watu 50 kufikia sasa wameaga dunia kutokana na sumu ya Lead na watoto zaidi ya 30 pia wamefariki.
Wakati huohuo baadhi ya waathiriwa hao wanasema wanaendelea kupitia hali ngumu ya kimaisha na serikali inaendelea kuwapuuza na kutaka mikakati kuwekwa ili wapate haki.
Kwa upande wake afisa wa dharura katika shirika la kutetea haki za kibinadamu la MUHURI kaunti ya Mombasa Francis Auma pamoja na wanaharakati wengine wamesema wataendelea kuwatetea wenyeji hao licha mahakama hiyo kuhairisha tarehe ya kutoa uamuzi dhidi ya kesi hadi wapate haki.
WENYEJI WA MTAA WA OWINO UHURU KAUNTI YA MOMBASA WAENDELEA KUDAI HAKI YAO
